Jumapili , 11th Jan , 2015

Timu za Simba na Mtibwa zitakutana katika mchezo wa Fainali wa Kombe la Mapinduzi utakaopigwa kesho katika dimba la Aman Zanzibar

Katika mechi za Nusu Fainali, Mtibwa Sugar ilifanikiwa kuitoa JKU ya Zanzibar kwa mikwaju ya Penati ya 4-3 baada ya sare ya 0-0 ndani ya Dakika 90, mechi iliyochezwa Uwanja wa Amaan, Zanzibar.

Katika Dakika 90 za mchezo,timu zote zilishambuliana kwa zamu, ambapo Mtibwa Sugar ilipoteza nafasi tatu za wazi za kufunga kupitia kwa Ame Ally, Mussa Mgosi na Ally Shomary.

Katika Mikwaju ya Penati waliofungwa kwa upande wa Mtibwa Sugar ni Ally Shomary, Henry Joseph, Ramadhan Kichuya na Vicent Barnabas huku kwa Upande wa JKU waliopata Penati wakiwa ni Isihaka Othman, Issa Khaidary na Khamis Abdallah.

Kwa Upande wa Simba iliibuka na bao 1-0 dhidi ya Polisi ya Zanzibar, Uwanja wa Amaan, Zanzibar bao pekee lililofungwa na Winga Ramadhan Singano 'Messi' katika dakika ya 26 ya mchezo.

Katika kipindi cha pili, Simba walirudi kwa kasi na Dakika ya 46 Dan Sserunkuma alikosa bao la wazi akiwa amebaki yeye na kipa baada ya kutanguliziwa pasi nzuri na Said Ndemla aliyeibuka nyota kwenye mchezo huo.

Ibrahim Hajibu naye aliyetokea Benchi kipindi cha pili akibadilishana na Elias Maguli, alikosa bao la wazi dakika ya 48 baada ya Pasi nzuri ya Jonas Mkude ambapo kipa alifanikiwa kuudaka Mpira..

Simba iliendelea kung'ara mchezoni na kupoteza nafasi zaidi ya kufunga kutokana na washambuliaji kutokuwa makini.