Jumatatu , 3rd Aug , 2020

Klabu ya Simba imeelezea masikitiko yake juu ya uvumi unaoenea mitandaoni kuwa itamfukuza kocha wao mkuu Sven VanDenBroeck mara tu baada ya msimu kumalizika.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa klabu ya Simba, Haji Manara (Pichani)

Akizungumza na EATV Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa wekundu hao Haji Manara amesema hakuna taarifa rasmi kutoka ndani ya klabu yao iliyozungumzia masuala ya mwalimu wao bali wanashangazwa na baadhi ya Waandishi wa Habari kuandika na kuzungumza uzushi juu ya kocha wao.

Manara amesema taarifa hizo zinawachonganisha wao na benchi la ufundi pamoja na wachezaji ambao kwa nyakati tofauti wanazisoma na kuzisikia katika vyombo vya Habari wakiamini kwamba huenda timu hiyo itawaacha mara baada ya mchezo wa Shirikisho.

Uongozi wa Simba umesema utawachukulia hatua watu wanaotumia kalamu zao kuwachonganisha kwa kuwa wametengeneza msingi mzuri wa kutoa taarifa kwa usahihi hivyo hawapo tayari kuchafua taswira ya klabu yao.

Ikumbukwe mara baada ya mchezo dhidi ya Namungo, Kocha wa Simba Sven Vandenbroeck alinukuliwa akisema hajui hatma yake iwapo ataendelea kuifundisha klabu hiyo au ataondoka kwa kuwa hata yeye ripoti za kuwa huenda akaondolewa anaziona mitandaoni.

Simba imewasili jijini Dar es salaam ikitokea mkoani Rukwa ambapo ilicheza mchezo wa Fainali wa kombe la Shirikisho dhidi ya Namungo ambapo ilishinda bao 2-1 na kutwa taji ambalo ni la tatu msimu huu ikiwa ni pamoja na la Ligi Kuu pamoja na Ngao ya Hisani.