Jumanne , 12th Feb , 2019

Kabla ya mchezo wa leo dhidi ya Al Ahly, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu ya Simba Mohammed Dewji aliitisha kikao cha bodi na kushauriana mambo mbalimbali huku wakitoka na maadhimio ya kuhamasisha mashabiki kujaa uwanjani.

Mashabiki wa Simba na Mohammed Dewji

Baada ya kikao hicho Mo Dewji aliitisha mkutano na wanahabari, ambao aliutumia kuwahimiza mashabiki kujaa uwanjani na kuipa nguvu timu yao ili iweze kushinda mchezo wao jambo ambalo limetimia.

Akiongea baada ya mchezo wa leo Mo Dewji amewashukuru mashabiki wa Simba kwa kujitokeza kwa wingi. ''Nawashukuru mashabiki wa Simba na mwenyezi Mungu''.

Mbali na Mo Dewji wengine waliojivunia ushindi wa leo ni mchezaji Erasto Nyoni, ambaye amesema ameshapona na ameanza mazoezi huku akiweka wazi kuwa ushindi wa leo umewapa nguvu zaidi ya kushinda mechi zilizobaki.

Kwa upande mwingine wasanii wakubwa nchini ambao ni mashabiki wa Simba akiwemo Mwana FA, JB, Mbunge Profesa Jay, Mwasiti na Monalisa kwa pamoja wametawala mtandao kwa shangwe juu ya ushindi huo.

Naye Waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba ametoa pongezi zake kwa Simba akiamini kuwa ushindi huo sio wa Simba pekee bali ni wa Tanzania nzima.