Ijumaa , 23rd Feb , 2018

Askari Polisi mmoja nchini Hispania amefariki kwa mshituko wa Moyo baada kuanguka wakati akijaribu kutuliza ghasia za mashabiki kwenye mchezo wa EUROPA kati ya Athletic Bilbao na Spartak Moscow jana usiku.

Askari huyo wa kiume aliyetambulika kwa jina la Inocencio Arias Garcia, alikuwa na umri wa miaka 50. Baada ya Garcia kuanguka wakati wa vurugu hizo nje ya uwanja wa San Mames,  kabla ya mchezo  alikimbizwa Hospitali lakini tayari alikuwa ameshapoteza maisha.

Shirikisho la soka nchini Hispania RSFF pamoja na Rais wa La Liga Javier Tebas, wametoa pole kwa familia ya Garcia pamoja na kukemea vitendo vya vurugu michezoni huku wakitaka vyombo vya usalama kuwashughulikia mashabiki waliohusika katika tukio hilo.

Katika vurugu hizo zilizohusisha makundi ya mashabiki wa timu za FC Spartak Moscow na Athletic Bilbao imeripotiwa kuwa mashabiki watatu wa Kirusi na afisa mmoja wa polisi walipelekwa hospitali baada ya kujeruhiwa.

Katika mchezo huo wa marudiano ulimalizika kwa Bilbao iliyokuwa nyumbani kwenye uwanja wa San Mames kukubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Spartak lakini imefanikiwa kusonga mbele kwa jumla ya mabao 4-3 baada ya kushinda 3-1 kwenye mchezo wa kwanza.