Jumatano , 11th Jul , 2018

Baada ya tetesi kueleza kuwa klabu ya soka ya Kagera Sugar, imewasajili wachezaji watano kutoka klabu ya Ndanda FC ya Mtwara, timu hiyo ya mkoani Kagera imeshindwa kuthibitisha taarifa hizo.

Kocha wa Kagera Sugar Meck Mexime

Akiongea na www.eatv.tv kocha mkuu wa Kagera Sugar Meck Mexime, amesema hajui lolote kuhusu usajili huo kwani hayupo na timu muda mrefu kwahiyo yote yanawezekana huenda wamesajiliwa au hawajasajiliwa.

''Mimi sijui kuhusu huo usajili, nachoweza kusema timu inafanya usajili lakini kwa hawa wachezaji watano kutoka Ndanda FC sina taarifa nao maana sikuwepo kwenye timu muda mrefu'', - amesema.

Tetesi zilizosambaa mitandao ni kuhusu wachezaji Jeremiah Kasubi ambaye ni mlinda mlango, walinzi Hemed Khoja, Ahmad Waziri, kiungo Majid Khamis na mshambuliaji Omary Mponda wote wakidaiwa kuikacha Ndanda FC na kusaini Kagera.

Kagera Sugar ambayo ilikuwa ikifanya vizuri katika misimu ya nyuma kwenye ligi kuu Tanzania Bara kiasi cha kumaliza kwenye nafasi 4 za juu, msimu uliopita haikuwa na msimu mzuri baada ya kumaliza katika nafasi ya 9 ikishinda mechi 8 kati ya 30 na kupoteza 9 pamoja na sare 13.

Jitihada za kuwatafuta viongozi wa Ndanda FC kulizungmzia hilo zimekwama baada ya kushindwa kupokea simu zao kila walipotafutwa.