Jumamosi , 21st Mei , 2016

Kila jambo ukitaka lifanyike kwa ufanisi basi lazima kuwe na mbinu mbadala za kufanikisha jambo husika na hili limeonekana katika michuano ya shule za Sekondari UMISETA Wilaya ya Kinondoni iliyoanza hapo jana katika viwanja vya shule ya Makondo Sec.

Baadhi ya wanamichezo wa shule za Sekondari wakipita kwa maandamano katika moja ya michuano ya UMISETA.

Michuano ya shule za Sekondari wilaya ya Kinondoni mkoa wa Dar es Salaam ambayo jana imeingia katika siku ya pili imeonekana kuwa na ushindani mkubwa katika kila mchezo kwa wachezaji wa timu hizo kuchuana vikali kutetea timu zao na hivyo kuibua ushindani mkubwa.

Mratibu wa michuano ya UMISETA mkoa wa kielimu wa Kinondoni Juma Hamad Nchimbi amesema timu zimekuwa zikionyesha mchezo mzuri na waushindani wa hali ya juu ni kutokana na kuja katika hatua hiyo zikiwa fiti kutokea katika michuano ya shule zao kimajimbo hivyo hali ya utimamu wa miili ya wachezaji iko sawa na kuwafanya kuweza kushindana katika kila mchezo.

Nchimbi amesema waliamua safari hii kuwachezesha katika majimbo yao kila shule inakotoka ili kupata timu za kila jimbo zenye uwezo wa kushindana na kutoa changamoto kubwa kwa timu nyingine zote shiriki tofauti na zamani michuano hiyo ilikuwa ikitawaliwa zaidi na Makongo Sekondari ambayo imejikita katika michezo na hivyo kuwa bingwa wa michuano hiyo kila msimu na hata kutoa idadi kubwa ya wachezaji wa kuunda kombaini ya Wilaya hadi Taifa.

Nchimbi amemaliza kusema kwa hali ilivyo ya ushindani wa timu zote katika kila mchezo wanataraji kupata timu bora ya kombaini ya Wilaya ya Kinondoni ambayo si kutoa changamoto kwa Wilaya zingine za Temeke na Ilala katika michuano ya Mkoa bali kuchukuwa ushindi katika fainali za michezo yote na kuwa bingwa wa jumla wa mkoa.

Kubwa Nchimbi amesema wanauhakika kwa asilimia kubwa timu itakayoteuliwa na jopo la ufundi la wataalamu katika michuano hiyo itakuwa ni timu bora ambayo pamoja na kufanya vema katika michuano ya mkoa wa Dar es Salaam itakayofanyika baadaye mwaka huu lakini pia wanataraji idadi kubwa ya wachezaji watakaounda kombaini ya mkoa wa Dar es Salaam watatoka katika kombaini ya Kinondoni.