Jumatano , 1st Apr , 2015

Kikosi cha wachezaji wa Zamani wa timu ya Fc Barcelona kinatarajia kuwasili nchini nchini Aprili saba mwaka huu ambapo wataanza na ziara visiwani Zanzibar wakiwa na lengo la kukuza vipaji vya vijana visiwani humo.

Akizungumza jijini Dar es salaam, Mmoja wa waratibu wa ziara ya magwiji hao, Said Tully amesema, msafara huo utakaokuwa na jumla ya watu 28 ambapo ni wachezaji 23 pamoja na viongozi watano utatanguliwa na mwanandinga wa zamani wa Uholanzi Johan Cruyff ambaye atakuwa kocha mkuu wa kikosi hicho.

Tully amesema baada ya ziara ya siku mbili visiwani Zanzibar, wachezaji hao watarejea jijini Dar es salaam kwa ajili ya maandalizi ya mechi ya kirafiki dhidi ya wachezaji wa zamani wa Tanzania itakayochezwa April 11 Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Tully amesema, ziara hiyo itakuwa na manufaa kwa watanzania kwani itasaidia kukuza vipaji kwa vijana pamoja na kuwapa mafunzo wachezaji wa zamani juu ya baada ya kustaafu soka ni kitu gani wanatakiwa kufanya.