Jumamosi , 24th Apr , 2021

Mabingwa wa Tanzania bara Simba SC wamekwea mpaka kileleni mwa msimamo wa ligi kuu Tanzania bara kwa mara ya kwanza msimu huu, baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Gwambina na kufikisha alama 58.

Mfungaji wa bao la pekee kwenye mchezo huu Mohamed Hussein

Bao pekee la mchezo huo limefungwa na mlinzi wa kushoto wa Simba Mohamed Hussein dakika ya 29. Kwa ushindi huu wekeundu wa msimbazi wanapanda kutoka nafasi ya pili mpaka ya kwanza na wanafikisha alama 58 ikiwa ni alama moja zaidi ya Yanga walio nafasi ya pili wakiwa na alama 57.

Ushindi huu wa Simba unawafanya mabingwa hao watetezi wa VPL kukusanya alama zote 9 kwenye michezo mitatu ya kanda ya ziwa, kabla ya mchezo wa leo michezo miwili iliyopita ya kanda ya ziwa walizifunga timu za Mwadui kwa bao 1-0, na wakaibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Kagera Sugar.

Baada ya kupoteza mchezo wa hii leo  Gwambina wanapoteza mchezo wa tatu mfululizo na wanasalia nafasi ya 12 wakiwa na alama 30.