Alhamisi , 8th Apr , 2021

Afisa mtendaji mkuu wa klabu ya Simba, Barbara Gonzalez amesema licha ya kufanikiwa kutinga hatua ya robo fainali ya michuano ya klabu bingwa Afrika, lakini mchezo wao wa kesho Aprili 9, 2021 dhidi ya Al Ahly ya Misri utakuwa ni wa kupambana kupata matokeo mazuri ili kulinda heshima.

Afisa Mtendaji wa klabu ya Simba, Barbara Gonzalez.

Barbara amesema “Cha msingi mechi yetu ya Ijumaa ni mechi ya heshima ni kweli tumeingia robo fainali lakini tunahitaji kutoka na alama hapa Cairo tutalinda heshima yetu na kulinda ukubwa na uzito wa timu yetu na pia inawatengeneza soka la wachezaji wetu”

“Cha msingi wachezaji wapambane kama fainali” Akamalizia Barbara.

Simba ambao ni wawakilishi pekee wa Tanzania kwenye michuano ya klabu bingwa Afrika, itacheza mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi dhidi ya Al Ahly Ijumaa ya kesho ikitaraji kuwa saa 2:00 usiku kwa saa za Afrika Mashariki kwenye dimba la Al Salaam ni si uwanja wa Cairo International.

(Wachezaji wa Simba wakifanya mazoezi kwenye uwanja wa Al Salaam nchini Misri usiku wa jana.)

Akizungumzia mabadiliko hayo ya uwanja, CEO amesmea:

“Leo tumeongea na mratibu mkuu ametoa sababu kwamba kwenye uwanja wa Cairo, klabu ya Zamalek watakuwa na mchezo Jumamosi uwanja wa Cairo , siku moja kabla ya mechi lazima waufanyie mazoezi maalum.

“Kwahiyo walikubaliana kwa pamoja nani atacheza wapi na Al Ahly wameamua na watu wa CAF wahamie uwanja wa Al Salaam ili kusiwe na mgongano kwenye kufanya mazoezi”

Simba ni kinara wa kundi lake, kundi A akiwa na alama 13, Al Ahly ipo nafasi ya pili ikiwa na alama 8 zote zikiwa zimefuzu ilhali AS Vita ya DR Congo ipo nafasi ya tatu ikiwa na alama 4 na Al-Merrik inashika mkia ikiwa na alama 2 huku zikishindwa kufuzu robo fainali.