Jumatatu , 30th Jan , 2023

Rais wa Shirikisho la Soka nchini Tanzania ‘TFF’ Wallace Karia amempongeza Murtaza Mangungu kwa kuchaguliwa kwa mara nyingine kuwa Mwenyekiti wa Simba SC.

Simba SC jana Jumapili (Januari 29) ilifanya Mkutano Mkuu wa Wanachama ulioambatana na Uchaguzi wa viongozi katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere ‘JINCC’ jijini Dar es salaam.

Rais Karia ametoa pongezi hizo kwa Mangungu kupitia taarifa rasmi iliyotolewa kwenye kurasa za Mitandao ya Kijamii za TFF.

Karia amesema kuchaguliwa kwa kiongozi huyo kwa mara nyingine tena, imeonesha namna ambavyo Wanachama wa Simba SC wana imani na utendaji wake.

Aidha kiongozi huyo wa TFF, amewapongeza Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba SC waliochaguliwa kupitia Uchaguzi Mkuu, huku akiahidi shirikisho la Soka nchini litaendelea kutoa ushirikiano na klabu hiyo kwa maendeleo mpira wa miguu nchini.

Ameongeza kuwa TFF inaamini chini ya Uongozi wao, na klabu ya Simba SC itaendelea kufanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa Barani Afrika (CAFCL), ambako kwa sasa wapo katika hatua ya makundi ili kuendelea kuipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa.

Katika uchaguzi huo ambao matokeo yake yametangazwa leo Jumatatu (Januari 30) Afajiri, Kaluwa amepata kura 1,045 huku Mangungu ambaye alikuwa anatetea kiti chake akipata jumla ya kura 1,311.

Kwa upande wa Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi walioshinda ni Dr Seif Ramadhan Muba (1636), Asha Baraka (1564), CPA Issa Masoud Iddi (1285), Rodney Chiduo (1267) na Seleman Harubu (1250).

Jumla ya Wanachama Simba SC waliopiga Kura ni 2363 Kura halali, lakini Kura halali zilikuwa 2356.