Alhamisi , 28th Jul , 2022

Kocha Mkuu Timothy Kingu wa kikosi cha ndondi kinachoiwakilisha Tanzania kwenye mashindano ya Jumuiya ya Madola ambayo yameanza rasmi  Julai 28,2022 amemhakikishia Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan na watanzania wote kurejea na medali za ushindi kwenye mchezo huo

kikosi cha ndondi kinachoshiriki michuano ya jumuiya ya madola

Akizungumza katika kambi ya wachezaji hao jijini Birmingham, Uingereza amesema wachezaji wake wamepikwa vizuri na watapata hamasa ya kutosha tayari kwa ajili ya pambano lililopo mbele yao.

Aidha, amesema hamasa kubwa inayotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan na Waziri anayesimamia Michezo nchini, Mhe Mohamed Mchengerwa na wadau mbalimbali kwa sasa zinawafanya wawe na ali na nguvu zaidi ya kushindana kufa na kupona kwenye mashindano haya.

Hadi sasa, tayari Mabondia wawili wa Tanzania Yusuf Changarawe na Kassim Mbundwike wameingia robo fainali za mchezo ya Jumuiya ya Madola inayoanza rasmi leo jijini Birmingham, Uingereza.

Bondia wa tatu wa Tanzania, Alex Isinde sio tu ataanzia mzunguko wa kwanza bali pia atakuwa ndiye Mtanzania wa kwanza kutupa kete kwenye mashindano hayo ya 48 ya nchi zilizopata kutawaliwa na Uingereza kesho Julai 29, 2022. 

Endapo wakishinda robo fainali wataingia nusu fainali ambako watawania kunyakua angalau medali za fedha.

Michezo ya Jumuiya ya Madola 2022 inazinduliwa rasmi leo saa mbili usiku kwa saa Uingereza (Tanzania iko mbele kwa saa mbili).

Tanzania itatupa tena kete zingine siku ya Jumamosi Julai 30, 2022 wakati wanariadha wanne wa mbio ndefu (Marathon) wanawake na wanaume wataingia kuchuana.

Wanariadha hao wa marathon ni Alphonce Simbu, Hamisi Misai, Jakline Sakilu na Failuna Matanga.

Kwenye michezo hiyo Tanzania inawakilishwa na wanariadha tisa, mabondia watatu, wacheza judo wawili, waogeleaji wawili na mnyanyua vitu vizito kwa walemavu