Jumamosi , 30th Jun , 2018

Jumla ya timu 15 zilizofanikiwa kushinda kwa tofauti kubwa ya pointi kwenye mechi za mchujo zilizofanyika leo kwenye viwanja vya JK Park Youth jijini Dar es salaam, zimetinga hatua ya 16 bora ya michuano ya Sprite Bball Kings mwaka huu.

Timu za Weusi Basketball Club (nyeusi) wamepata pointi wakichuana na Kichangani (blue).

Katika jumla ya mechi 24 zilizochezwa leo timu ya The Team Kiza ambayo ilicheza na Kijichi Warriors na kushinda kwa pointi 49 kwa 4, imeongoza kwa tofauti ya pointi ikiwa na faida ya 45 hivyo kufuzu 16 bora. 

Timu iliyoshika nafasi ya pili kwa tofauti kubwa ya pointi ni Stylers ambao walishinda kwa pointi 44 dhidi ya 6 za Denth Shoppers hivyo kuwa na faida ya pointi 38. Timu nyingine ni St. Joseph walioshinda pointi 42 dhidi ya 7 za Madena na kuwa na mtaji wa pointi 35.

Mbali na hizo timu nyingine zilizofuzu ni Oysterbay walioshinda kwa pointi  48 dhidi ya 19 za Ilala East Zone hivyo kuwa na tofauti ya pointi 29, wakifuatiwa na Flying Driblers ambao walishinda kwa alama 37 kwa 9 za Kurasini Warriors.

Timu hizo 15 zilizopatikana leo kwenye mchujo zitaungana na bingwa mtetezi Mchenga Bball Stars kukamilisha timu 16 zitakazocheza hatua ya 16 bora. Utaratibu na tarehe ya kuanza kwa hatua hiyo utatangazwa hivyo endelea kufuatilia vipindi vya East Africa TV na Radio pamoja na mitandao yetu.

Orodha kamili

1. The Team Kiza
2. Stylers
3. St. Joseph
4. Oysterbay
5. Flying Driblers
6. Portland
7. Raptors
8. Ukonga Hitmen 
9. Ukonga Warriors
10. Temeke Heroes
11. Water Institute
12. Fast Heat
13. Mbezi Beach KKKT
14. Air Wings 
15. DMI
16. Mchenga Bball Stars