Jumanne , 11th Jun , 2019

Klabu ya soka ya KMC ambayo msimu ujao 2019/20 itashiriki michuano mitatu tofauti kwa maana ya Ligi kuu Bara, Kombe la shirikisho nchini na Kombe la shirikisho barani Afrika, wameweka wazi aina ya wachezaji ambao wanawahitaji.

Meya wa Manispaa ya Kinondoni Benjamin Sitta, ambaye ni kiongozi wa juu wa timu hiyo, ameweka wazi kuwa watazingatia suala la nidhamu kwa wachezaji watakaowasajili.

"Ukweli ni kwamba wachezaji wetu wa kitanzania bado wanatatizo la nidhamu na malengo. Tunachotaka sisi ni kuwa na wachezaji wachache wa kigeni ambao watakuwa mfano kwa vijana wetu", amesema Sitta.

Aidha Sitta ameongeza kuwa, "Tunataka wachezaji tutakaokuwanao wengi watakuwa wakitanzania wenye vipaji na ni wadogo tunaamini tutafanya vizuri sana."

KMC inaungana na timu za Simba, Azam FC na Yanga kuiwakilsiha Tanzania kimataifa ambapo itacheza, Azam FC na KMC zitacheza kombe la shirikisho huku Simba na Yanga zikishiriki Ligi ya Mabingwa.