Jumanne , 20th Mei , 2014

Baraza la Taifa la Hifadhi na usimamizi wa Mazingira nchini Tanzania (NEMC) limelalamikia mchakato wa kutoa hati ya tathimini ya athari ya mazingira kwamba unachukua muda mrefu.

Uvunaji holela wa rasilimali za misitu kama unavyoonekana hapo juu umekuwa ukipingwa vikali na baraza la taifa la usimamizi wa mazingira NEMC.

Mkurugenzi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma wa NEMC, Vedasto Makoti, ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam ambapo amesema kuwa kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wawekezaji kuwa muda unaotumika kutoa hati hizo ni jumla ya siku 149 ambazo hutumika kufanya maamuzi tu.

Makoti ameongeza kuwa sheria haijampangia mwekezaji muda gani mtaalam-mwelekezi wake atumie wakati wa utafiti, na kuwa kumekuwepo na ukomo wa bajeti na uchache wa wataalam wa kufanya ufuatiliaji na hivyo kuufanya kuwa hafifu.

Wakati huo huo, Mwanasheria wa NEMC Machare Heche ametoa wito kwa wananchi kutunza mazingira na kuwasilisha taarifa kwa baraza kuhusu uharibifu au uchafuzi wa mazingira katika maeneo wanayoishi.