Ijumaa , 19th Nov , 2021

Mazungumzo ya mkataba mpya baina ya Manchester United na winga wake Jesse Lingard yamekwama baada ya pande zote mbili kushindwa kufika muafaka huku kandarasi ya mchezaji huyo ikifikia tamati mwezi Juni mwakani 2022 .

(Winga wa Manchester United, Jesse Lingaard)

Lingard alitolewa kwa mkopo kuelekea klabu ya West Ham United msimu uliopita na kuonesha kiwango cha hali ya juu huku  alitazamiwa kupata nafasi ya kutosha kwenye kikosi cha Ole Gunnar Solskjear msimu huu lakini mambo yameendea ndivyo sivyo.

Mchezaji huyo ameanza kwenye mchezo mmoja tu ambao ulikuwa mwezi Septemba 22 mwaka huu kwenye kombe la Carabao dhidi ya West ham ambapo United waliofungwa 1-0 na akiingia kama mchezaji mbadala kwenye mechi saba za misimu huu kwenye mashindano yote na kucheza jumla ya dakika 76 kwenye mitanange hiyo.

Inafahamika kuwa chini ya hali hiyo, Lingard, ambaye amekuwa  na United tangu akiwa na umri wa miaka saba, haoni umuhimu wa kutafuta mazungumzo zaidi na ana matumaini ya kupata uhamisho wa mkopo mwezi Januari 2022 kabla ya kuondoka kwa uhamisho huru mwisho wa msimu huu wa mwaka 2021/2022.