Monday , 2nd Nov , 2015

Ikulu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekana kupokea maombi ya Maalim Seif Sharrif Hamad kutaka kuonana na Rais Jakaya Kikwete ili kuzungumzia suala la Mgogoro wa Kisiasa Visiwani Zanzibar.

Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akifanya mazungumzo na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Shariff Hamad aliemtembelea Ikulu May 30,2015

Taarifa ya Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu iliyotolewa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana ilieleza kuwa imesikitishwa na madai ya maalim Seif huku ikieleza kuwa sio ya Kweli.

Taarifa hiyo imesema kuwa kile ambacho raisi Kikwete amekipokea ni malalamiko ya CUF kuhusu baadhi ya vitendo kutoka kwa baadhi ya askari wa jeshi la polisi Zanzibar na ombi kwa ajili ya kuwezesha mazungumzo kati ya maalim Seif na Mkuu wa Majeshi Davis Mwamunyange.

Hata hivyo taarifa hiyo imeongeza kuwa Rais Kikwete amemuagiza Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Ernest Mangu kuchunguza madai hayo ya CUF na kumpelekea taarifa juu ya uchunguzi huo.

Aidha taarifa hiyo inasema kuwa Rais Kikwete amekua akiguswa na hali ya kisiasa na Usalama wa Zanzibar kama ilivyo kwa watanzania wengine na amekuwa akifanya kazi bila kuchoka huku akipata ushauri wa kina juu ya kilichotokea Zanzibar.