Sunday , 9th Apr , 2017

Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad amesema ameiandikia hazina pamoja na Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuwa kamwe upande anaouongoza hautahusika na pesa yoyote inayotolewa na kutumika katika kipindi hiki.

Maalim Seif Sharif Hamad

Ameitaka Hazina kustisha utoaji wa pesa kwa chama hicho katika kipindi hiki ambacho chama hicho kipo katika mvutano wa kiuongozi unaoonekana kuwa ni mgogoro huku akisema huwa chama hicho hakina mgogoro bali kipo katika hujuma zenye nia ovu.

Akizungumza katika mkutano wake na wanahabari jijini Dar es Salaam leo, Maalim Seif pia amehoji mazingira yanayotumiwa kuruhusu kutolewa kwa ruzuku hizo (Milioni 369) tena kupitia akaunti ya mtu binafsi na kutolewa ndani ya kipindi cha siku moja kinyume na taratibu za kifedha.

Akifafanua kuhusu suala hilo, Maalim Seif amesema kumekuwa na mazingira yanayotia shaka juu ya matumizi ya pesa za chama, huku akihoji ni kwa nini vyombo vya dola havikufuatilia uhamishwaji na baadaye utolewaji wa kiasi kikubwa cha pesa katika kipindi kifupi kinyume na taratibu.