Saturday , 5th Sep , 2015

Serikali ya Tanzania imesema ujenzi wa taasisi ya magonjwa ya moyo na uzibaji wa matundu iliyopo katika hospital ya taifa ya muhimbili umesababisha serikali kuokoa zaidi ya shilingi bilioni 2.5 ambazo zingetumika kuwasafirisha nje ya nchi wagonjwa

Waziri wa afya na ustawi wa jamii Dkt. Seif Rashid

Hayo yameelezwa leo jijini Dar es salaam na Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na waziri wa afya na ustawi wa jamii Dkt. Seif Rashid wakati wa uzinduzi wa taasisi hiyo iliyopewa jina la The Jakaya Kikwete Cardiac Institute

Dkt. Seif Rashid amesema serikali sasa itaendelea kuboresha sekta mbali mbali za afya lengo likiwa ni kuhakikisha watanzania wanapata huduma bora na kuachana na kwenda nje ya nchi kwa kupata matibabu.

Dkt. Seif amesema kuwa tangu mwezi Januari hadi August taasisi hiyo imekwishawahudumia zaidi ya wagonjwa 14,000 wa nje huku wagonjwa waliolazwa ni 912 na kufanya upasuaji kwa wagonjwa 148 ni wagonjwa watano tu waliofariki ikiwa ni sawa na asilimia 3.

Kwa upande wake mkuu wa taasisi hiyo amesema taasisi hiyo itaendelea kutoa huduma ya ubadilishaji wa mishipa ya moyo, moyo kupanuka, mishipa ya moyo kuziba na mapigo ya moyo kushuka.