Sunday , 17th Jul , 2016

Mkurugenzi wa shirika la kusaidia na kutetea haki za wanawake na makundi maalum nchini Bi Mary Lusimbi amesema wameamua kuwasaidia wanawake kupata haki zao kikamilifu ili kupinga dhana ya wanawake kuwa tegemezi kila wakati.

Bi Lusimbi ameyasema hayo katika mahojiano maalum na East Africa Radio ambapo amesema kuwa sambamba na kuwawezesha wanawake mbalimbali nchini pia wamewajumuisha na vijana kutoka mikoa mbalimbali ili kuhakikisha wanawainua kiuchumi na kuacha utegemezi wa kipato.

Amesema wanashirikiana na mashirika mbalimbali duniani katika kutoa ruzuku ambayo itasaidia kuwawezesha kufanya biashara mbalimbali ambazo wana lengo la kuzifanya kinamama hao na kujikwamua zaidi ili kufikia kipato cha kati.

Kwa upande wake mwalimu wa wajasiriamali hao Rose Julius amekemea tabia ya wanawake ambao wanaamini hawawezi kufanya mabadiliko bila kuwa na nguvu ya zaidi na kuwataka wajiamini katika utekelezaji wa majukumu yao.

Aidha wameiomba serikali kurudisha kwa haraka swala la mchakato wa katiba mpya ili kubadilisha baadhi ya mitazamo ambayo imezoeleka kwa wanawake na jamii kwa ujumla.