Thursday , 15th Dec , 2016

Serikali imewataka wamiliki wa nyumba mkoani Dar es Salaam ambao nyumba zao zina wapangaji, kuhakikisha wanakuwa na picha za wapangaji wao wote ili kuwatambua na kupunguza uwezekano wa kuhifadhi wahalifu.

Baadhi ya wahamiaji haramu waliowahi kukamatwa mkoani Ruvuma

Agizo hilo limetolewa leo na Kamishna wa Uhamiaji Kanda ya Dar es Salaam John Msumule mara baada ya kufanya oparesheni ya kufunga madanguro na kuwasaka raia wa kigeni wanaoishi nchini kinyume cha sheria.

Msumule pia amewaonya watu wanaowaajiri raia wa kigeni bila vibali, kuoa ama kuolewa na raia wa kigeni bila vibali kufika katika ofisi za uhamiaji na kufuata utaratibu wa kisheria wa wao kuishi nchini ili kuondokana na usumbufu utakaojitokeza pindi watakapo chukuliwa hatua za kisheria.

Pia amesema kuwa, tayari wamewakamata waajiri na waajiriwa wa kampuni ya Jantu Constraction Company ambayo imewaajiri raia wa kigeni bila ya kuwa na vibali vya kuishi nchini Tanzania.