Saturday , 18th Oct , 2014

Bodi ya ligi Tanzania bara TPLB imewataka wadau wa soka, makampuni na taasisi mbalimbali kujitokeza kudhamini ligi daraja la kwanza ambayo inaendelea hivi sasa katika maeneo mbalimbali hapa nchini

Timu za daraja la kwanza zikiwa zimejipanga kusubiri ukaguzi kabla ya mchezo

Mtendaji mkuu wa bodi hiyo Silas Mwakibinga amesema ligi daraja la kwanza ni moja ya ligi bora hapa nchini hivyo ili kuinua soka ni wakati sasa wa ligi hiyo kupata udhamini wa ligi nzima, waamuzi au timu moja moja kama ilivyofanya manispaa ya Kinondoni kwa timu ya TESEMA,

Wakati huo huo shirikisho la soka nchini TFF limefanya mabadiliko katika ya mechi Nne za Kundi A la Ligi Daraja la Kwanza (FDL) zimefanyiwa marekebisho ili kutoa fursa ya matumizi ya Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam.

Timu za African Lyon na Kimondo FC ambazo awali zilikuwa zicheze Oktoba 25 mwaka huu kwenye Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani, sasa zitacheza Oktoba 26 mwaka huu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

Nayo mechi ya Polisi Dar es Salaam na Majimaji ya Songea iliyokuwa ichezwe Oktoba 26 mwaka huu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, sasa itachezwa Oktoba 27 mwaka huu kwenye uwanja huo huo.

Mechi ya Friends Rangers na Ashanti United iliyokuwa ichezwe Mabatini mkoani Pwani, Oktoba 26 mwaka huu, sasa itachezwa Uwanja wa Karume, Oktoba 28 mwaka huu.

Pia mechi ya Lipuli FC na JKT Mlale iliyokuwa ichezwe Oktoba 25 mwaka huu kwenye Uwanja wa Samora mjini Iringa, imesogezwa mbele kwa siku moja. Mechi hiyo sasa itachezwa Oktoba 26 mwaka huu kwenye uwanja huo huo.