Thursday , 26th Feb , 2015

Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) imethibitisha kushiriki michuano ya kombe la COSAFA nchini Afrika Kusini kufuatia mwaliko wa Baraza la vyama vya soka Kusini mwa Afrika (COSAFA).

Michuano ya kombe la COSAFA inatarajiwa kuanza kutimua vumbi katikati ya mwezi Mei mwaka huu nchini Afrika Kusini, na ratiba ya hatua ya awali ya makundi inatarajiwa kutangazwa leo saa 1:00 kamili jioni kwa saa za Afrika Mashariki.

Taifa Stars itakuwa juu (seeded) katika hatua ya makundi, ambapo nchi nane zitagawanya katika makundi mawili na washindi wa kila kundi wataingia hatua ya robo fainali, nchi nyingine zitakazoanzia kwenye makundi ni Lesotho, Madagascar, Marutius, Namibia, Seychelles, Swaziland.

Katika kila kundi, timu zote zitacheza michezo mitatu na mshindi wa kila kundi ataingia katika hatua inayofuata ya robo fainali itakayozijumuisha nchi za  Afrika Kusini, Botswana, Ghana, Malawi, Msumbuji na Zambia ambazo zimeingia katika hatua ya pili kutokana na nafasi zao kwenye msimamo wa viwango vya FIFA.

Kombe la COSAFA lilianza mwaka 1997 linajumuisha nchi 16 wanachama kutoka Kusini mwa Bara la Afrika, limekuwa likifanyika kwa kushirikisha nchi wanachama waliopo Kusini mwa bara la Afrika.

Nchi wanachama wa COSAFA ni Afrika Kusini, Angola, Botswana, Comoros, Lesotho, Madagascar, Malawi, Maurtius, Mayotte, Msumbuji,Namibia, Reunion, Sychelles, Swaziland, Zambia na Zimbabwe.