Monday , 6th Feb , 2017

Bondia Mohammed Matumla amekumbana na kipigo kisicho cha kawaida na kuumizwa vibaya katika pambano la ngumi, hali iliyosababishwa akimbizwe katika hospitali ya Temeke kwa kutumia gari dogo la mizigo au 'pick up'.

Mabondia Mafaume Mfaume kushoto na Mohamed Matumla wakitunishiana misuli kabla ya mpambano huo.

Matumla ambaye ni mtoto wa bondia nyota wa zamani, Rashid Matumla amepigwa katika raundi ya saba na bondia Mfaume Mfaume katika pambano la utangulizi.

Matumla alianza kupoteza mwelekeo katika raundi ya tano lakini akajitutumua hadi raundi ya saba ambayo aliambulia kipigo kikali kutoka kwa Mfaume.

Baada ya kusukumiwa ngumi mfululizo, alianguka lakini akaonekana ni kama mtu aliyechanganyikiwa, akitaka kukimbia, lakini alizuiliwa na baadaye kulazwa chini kwa ajili ya huduma.

Daktari aliyekuwa mtazamaji, ndiye alilazimika kumtibu kwa ajili ya huduma ya kwanza kwa kuwa hakukuwa na huduma ya kwanza wala gari la wagonjwa ukumbini hapo.