Thursday , 21st May , 2020

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, ameyataja maduka ambayo yameridhia kufanya punguzo la bei za nguo hadi asilimia 80, lengo likiwa ni kuwawezesha wananchi wake kupendeza siku ya kilele cha siku tatu za maombi ya shukrani, zilizotangazwa na Rais Magufuli.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda.

Makonda ametangaza punguzo hilo la bei leo Mei 21, 2020, na kuyataja maduka hayo ambayo ni pamoja na Mr Price, Red Tag ya Mlimani City, Vunja Bei, maduka ya nguo yaliyopo City Mall pamoja na maduka mengine yaliyopo Posta, Kariakoo, Kinondoni na Sinza.

Aidha Makonda amesema kuwa anatamani kuona kila mwananchi ndani ya Mkoa huo, anasherehekea vyema siku ya Jumapili kama sehemu ya shukrani kwa Mungu, kuwakinga watu wake na maambukizi ya Virusi vya Corona na baada ya hapo kila mtu atapaswa kuchapa kazi.

Lakini wamiliki wa maduka hayo nao, hawakuwa nyuma kuwaomba wananchi kujitokeza kwa wingi kufanya manunuzi, huku wakimpongeza RC Makonda kwa kuwapigania wananchi ili kuhakikisha wanapata mavazi mazuri kwa bei nafuu.