Tuesday , 29th Dec , 2020

Kwa mara ya kwanza Mei 31, 2020, baadhi ya magari yalianza kupita kwenye barabara ya juu ya Ubungo, baada ya kuanza kutumika kwa ajili ya majaribio, barabara ambayo imeweza kubadili taswira nzima ya Jiji la Dar es Salaam na kupunguza msongamano wa magari.

Mwonekano wa Barabara za juu za Ubungo (Ubungo Flyover)

Mradi wa ujenzi wa daraja hilo ulijengwa na mkandarasi kutoka China, China Civil Engineering Construction Co-operation (CCECC), mradi ambao ulitoa ajira kwa asilimia 90 kwa Watanzania na asilimia 10 kutoka kwa raia wa kigeni na kuelezwa kuwa daraja hilo litawezesha magari zaidi ya 65, 000, yanayotumia makutano ya barabara za Morogoro, Sam Nujoma na Mandela kupita bila msongamano.

Awali kwa mujibu wa Mtendaji Mkuu wa TANROADS Mhandisi Patrick Mfugale, alisema kuwa mradi huo utagharimu zaidi ya bilioni 177, na kwamba fedha za mradi huo zingine ni za mkopo kutoka Benki ya Dunia  kwa ajili ya uboreshaji  miundombinu ya  usafiri Dar es Salaam.

Mkataba wa ujenzi wa mradi wa daraja la Ubungo ulisainiwa mwaka 2017 na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Mhandisi Patrick Mfugale, mkataba ambao ulikuwa unamtaka mkandarasi kukamilisha ujenzi huo ndani ya miaka mitatu na kiasi cha shilingi bilioni 2. 1, kililipwa kama fidia kwa wananchi waliopisha ujenzi huo.

Mnano Oktoba 8, 2020, Rais Magufuli, alitembelea katika barabara hizo za juu (Ubungo interchange), kwa lengo la kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara hizo.