Thursday , 7th Jan , 2021

Jeshi la polisi mkoa wa Arusha limesema kuwa Askari William Joseph, aliyekutwa na gongo, viroba, misokoto 20 ya bangi na kujiunganishia umeme nyumbani kwake kinyume cha utaratibu, amefukuzwa kazi kwa fedheha na jalada la kesi yake limepelekwa ofisi ya mashtaka kwa hatua zaidi.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, ACP Salum Hamduni

Taarifa hiyo imetolewa leo Januari 7, 2021, na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, ACP Salum Hamduni, na kusema kuwa tukio la Askari huyo kukutwa na vitu hivyo lilitokea Januari 5 mwaka huu mtaa wa Muriet jijini humo, mara baada ya mkuu wa wilaya hiyo Kenani Kihongosi na OCD kufanya msako na kumkuta na vitu hivyo.

Mbali na kukutwa na gongo, Askari huyo pia alikutwa na mafuata ya diesel lita 85, pakiti tatu za pombe aina ya kiroba, boksi 84 za viroba, ambavyo vilipigwa marufuku na serikali pamoja na kukutwa na vyuma vya bomba vilivyochakaa kinyume cha taratibu.

Mbali na hilo pia, Jeshi la Polisi limewafukuza kazi Askari wengine watatu, ambao walikamatwa kwa tuhuma za kushawishi na kupokea rushwa kutoka kwa mmiliki wa kampuni ya Germs and Rocks Ventures iliyopo jijini Arusha, ambao ni G. 5134 DC Heavenlight Mushi, H.125 DC Gasper Paul na H.1021 PC Bryton Murumbe.