Sunday , 14th Mar , 2021

Serikali imepiga marufuku wafungwa kutoka Magereza mbalimbali nchini kutumika katika kazi binafsi isipokuwa kwa kufuata utaratibu unaotambulika kisheria.

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Khamis Hamza Chilo akizungumza na askari kutoka Idara taasisi zilizopo chini ya wizara hiyo,mkoani Singida.

Marufuku hiyo imetolewa leo na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Khamis Hamza Chilo wakati wa kikao kilichojumuisha askari polisi kutoka Idara zilizopo chini ya wizara, mkoani Singida ambapo amesema wafungwa wana taratibu zao zinazowaongoza katika mfumo wao mzima wakiwa gerezani huku akiwaagiza wakuu wa magereza yote nchini kufuata taratibu hizo.

“Kuna taarifa za uhakika kwa wafungwa kutumika katika shughuli binafsi ikiwemo kujenga nyumba za watu binafsi na kulima mashamba ya watu binafsi, nimpongeze Kamishna Jenerali wa Magereza, Suleiman Mzee katika kipindi chake ameanza kuchukua hatua madhubuti kuhakikisha jeshi linarudi katika misingi yake na sasa tunaona magereza inaendelea kuboreka kila uchwao sisi kama serikali tunapiga marufuku matumizi binafsi ya wafungwa katika shughuli yoyote binafsi ila kwa kufuata utaratibu,” alisema Naibu Waziri Khamis Hamza Chilo

Sambamba na hilo amewataka wakae kwa pamoja kujitathimini na kupiga marufuku kurundika kwa mahabusu badala yake wapewe dhamana kwa mujibu wa sheria na taratibu.