Saturday , 28th Aug , 2021

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro, amewataka Watanzania ambao hawawezi kuzaa watoto wengi na kuwalea basi waache na sio kuzaa watoto wenye tabia kama za Hamza aliyewaua Askari Polisi kwa risasi Agosti 25, 2021.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro

Kauli hiyo ameitoa hii leo Agosti 28, 2021, wakati wa gwaride maalum la kuwaaga Makamishna wastaafu wa Jeshi hilo akiwemo Balozi Valentino Mlowola na Robert Boaz aliyekuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini.

"Niseme kwamba hiyo familia ya Hamza inajisikiaje, ungekuwa wewe ndiyo Baba au Mama yake Hamza ungejisikiaje kuzaa kwako wewe umetuletea balaa Watanzania, kwahiyo niwaombe watanzania wengine wasituzalie watoto kama Hamza," amesema IGP Sirro.

Aidha IGP Sirro amesema kwamba wao kama Jeshi la Polisi wameshakamilisha kuufanyia uchunguzi mwili wa Hamza na kazi iliyobaki ni kwa ndugu kuuchukua kwa ajili ya kuuzika na endapo wakichelewa basi utazikwa na Manispaa.