Sunday , 21st Nov , 2021

Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi wa kampuni ya klabu ya Simba, Abdallah Salim Mhene ‘Try Again’ amesema bodi na Uongozi wa klabu hiyo umeridhia kumpa Urais wa Heshima, Mohammed Dewji kutoka na mchango wake mkubwa.

(Mwekezaji wa Simba, Mohamed Dewji)

Try Again ameyathibitisha hayo wakati alipokuwa anaongea mbele ya wanachama na mashabiki wa Simba waliojitokeza asubuhi ya leo kwenye mkutano mkuu wa mwaka wa klabu hiyo uliofanyika katika ukumbi wa Mwl. Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti amesema, "Kwa kutambua mchango mkubwa, kwa makubwa aliyotufanyia kwenye klabu hii. Kwa mapenzi makubwa aliyonayo na klabu hii. Kwa uwekezaji mkubwa aliouwekeza kwenye klabu hii. Katika kikao cha bodi kilichokaa hivi karibuni, kupitia Ibara ya 50, bodi imeamua kumpa Urais wa heshima Ndugu, Mohammed Dewji"

Taarifa hiyo ilipokelewa na shangwe nyingi na wanasimba huku wakiliimba jina la Mwenyekiti wao wa zamani ya bodi hiyo ambaye ni mwekezaji mkuu wa klabu hiyo.