Monday , 14th Nov , 2022

Mkuu wa Wilaya ya Nyang'hwale Jamhuri William ameagiza  kusakwa kwa  wanafunzi zaidi ya 190 ambao hawakufanya mitihani ya Taifa ya kidato cha pili kwa sababu mbalimbali ikiwepo, mimba na kuozeshwa ili waweze kuendelea na masomo.

Wanafunzi wakifanya mtihani

William ametoa maagizo hayo kwa watendaji wa kata, maafisa elimu pamoja na  Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kwenye baraza la madiwani la halimashauri hiyo na kuwataka kuhakikisha wanawapata wanafunzi wote ambao hawakufanya mitihani hao pamoja na wote waliowasababishia.

"Nimeelekeza vilevile Tathmini ifanyike kwa kina ili kubaini ukubwa wa utoro katika madarasa mengine, shule za sekondari na shule za msingi ili hatua zichukuliwe." Amesema Mkuu wa Wilaya ya Nyang'hwale Jamhuri William 

Kwa upande wake afisa Elimu sekondari wa halmashauri hiyo Patrick Atanasy anaelezea mikakati waliyoiweka kuhakikisha wanawapata wote waliohusika.

"Utoro, kuzuiwa na wazazi na sababu zingine kama mimba, na mpaka sasa hivi mkakati uliopo ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kufanya msako kitongoji kwa kitongoji na nyumba kwa nyumba kuhakikisha kwamba tunawabaini watoto hao na wale waliosababisha watoto hao wasifike shuleni" amesema Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Nyang'hwale Patrick AtanasyAtanasy.

Baadhi ya viongozi wa halmashauri hiyo wamechukizwa na tukio hilo huku wakiomba msako ufanywe kwa haraka ili wanafunzi hao waweze kupatikana.