Monday , 14th Nov , 2022

Baraza la Mawaziri la serikali ya Tanzania limepokea taarifa ya awali ya ajali ya ndege ya Precision Air iliyotokea Novemba 6, 2022, Bukoba mkoani Kagera na kugharimu maisha ya watu 19.

Ndege iliyopata ajali

Kauli hiyo imetolewa hii leo Novemba 14, 2022, jijini Dodoma na Msemaji Mkuu wa serikali kufuatia maelekezo ya Baraza la Mawaziri lililoketi hii leo na Rais Samia Ikulu ya Chamwino.

"Leo kikao cha Baraza la Mawaziri kikiongozwa na Rais Samia kimekutana hapa Dodoma, na Baraza la Mawaziri limepokea taarifa ya awali ya ajali ya Ndege ya Precision Air na hatua zilizochukuliwa baada ya ajali," amesema Msigwa

Aidha Msemaji ameongeza kuwa "Baraza la Mawaziti limewaelekeza wataalam wa ndani kushirikiana na wataalam kutoka nje ya nchi katika kufanya uchunguzi na kupata chanzo cha ajali pamoja na kupata mapendekezo ya hatua zinazotakiwa kuchukuliwa mara baada ya ajali kutokea,".

Baraza la Mawaziri pia limeelekeza kwamba vitengo vyote vinavyohusika na kukabiliana na majanga nchini viimarishwe ili kuongeza uwezo zaidi wa kukabiliana na majanga yanapotokea.