Friday , 5th May , 2023

Aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Uttoh ametoa wito kwa taasisi zote zinazohusika kuchunguza yaliyozungumzwa kwenye ripoti ya CAG kuhakikisha wanakuwa wawazi 

CAG Mstaafu huyo akizungumza katika kipindi cha #SupaBreakfast ya #EastAfricaRadio amesema kuwa wananchi wanapenda kuona hatua zikichukuliwa na si vinginevyo

"Zile taasisi ambazo zina jukumu la kuchukua ripoti ya CAG na kuifanyia uchunguzi wa kina tuziombe zijitahidi kufanya kwa bidii, na hatua zinazochukuliwa jamani zisiwe za siri siri, wananchi wanafarijika wakijua kwamba hatua hii imechukuliwa kutokana na hiki" amesema Uttoh 

Katika hatua nyingine amekipongeza Chama cha Mapinduzi ambacho ndio Chama tawala kwa jinsi kilivyopokea na kuanza kuchukua hatua dhidi ya ripoti ya CAG huku akikiri kuwa huko nyuma utaratibu huo haukuwepo 

"Nafikiri kilichofanyika kwa ripoti ya CAG kupelekwa kwenye kamati kuu ya chama na kazungumzwa ni mara ya kwanza hili limetokea, kwa miaka 8 ya mimi kuwa CAG ripoti yangu ilikuwa inatoka sikusikia chama kinafanya ajenda, nikipongeze chama tawala" 

Hata hivyo amesema Ripoti ya CAG mwaka huu ni moja ya ripoti bora kwa kuwa imesheheni taarifa za uhakika
"Ripoti ya CAG mwaka huu ni nzuri sana, na uzuri wake ni ripoti ambayo wameifanyia masahihisho na ina makosa machache sana ukilinganisha na ripoti za nyuma, alafu umesheheni taarifa kubwa"