Friday , 5th May , 2023

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz anaendelea na ziara barani Afrika leo Ijumaa, kwa kufanya mazungumzo na Rais wa Kenya William Ruto mjini Nairobi. Kansela Scholz ameunga mkono Afrika kuwakilishwa katika kundi la G20.

Katika ziara yake nchini Kenya Kansela Olaf Scholz ameambatana na viongozi kadhaa wa makampuni ya biashara kutoka Ujerumani.

Mjini Nairobi amepokelewa na Rais wa Kenya William Ruto na mazungumzo ya kisiasa baina ya viongozi hao yatajikita juu ya matumizi ya nishati endelevu, kupanua uhusiano wa kibiashara na utatuzi wa migogoro.

Siku ya Alhamis Kansela huyo wa Ujerumani alitembelea makao makuu ya Umoja wa Afrika mjini Addis Ababa, ambapo alifanya mazungumzo na rais wa kamisheni ya umoja huo, Moussa Faki Mahamat.