Tuesday , 17th Jun , 2025

Takribani watu 15 wameuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa katika mashambulizi ya Urusi katika mji mkuu wa Ukraine Kyiv

Shambulio hilo lililotokea usiku wa kuamkia Jumanne lilikuwa mojawapo ya mashambulizi makubwa zaidi ya mabomu katika mji wa Kyiv tangu kuanza kwa uvamizi huo mkubwa zaidi ya miaka mitatu iliyopita.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ukraine, Ihor Klymenko, alisema jumla ya ndege zisizo na rubani 440 na makombora 32 yamerushwa nchini humo.

Wakati huo huo, vitengo vya ulinzi wa anga vya Urusi vilinasa na kuharibu ndege 147 za Ukraine usiku kucha, wizara ya ulinzi ya Moscow ilisema.

Shambulio huko Kyiv lilidumu zaidi ya saa tisa na kusababisha wakazi kukimbilia kwenye makazi ya chini ya ardhi kutoka kabla ya saa sita usiku hadi baada ya jua kuchomoza.

Maafisa walisema kombora la balestiki lilipiga jengo la ghorofa tisa katika wilaya moja, na jumla ya wilaya 27 za jiji hilo zikiteketea.

Milipuko mikubwa ilitikisa jiji hilo, pamoja na milio ya bunduki zinazotumiwa na vitengo vya ulinzi wa anga vya Ukraine kuangusha ndege zisizo na rubani.

Urusi imezidisha mashambulizi yake ya anga dhidi ya miji ya Ukraine katika wiki za hivi karibuni

Kyiv imeanzisha mashambulizi ya aina yake, kwani mazungumzo ya moja kwa moja kati ya pande zinazozozana yameshindwa kupata usitishaji mapigano au mafanikio makubwa.