Jumanne , 21st Jul , 2015

Jumla ya wanachama 109 wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Dodoma wamejitokeza kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya kuteuliwa kuwania nafasi za ubunge katika majimbo yaliyopo mkoani humo.

Katibu wa CCM mkao wa Dodoma Albart Mgumba akikata utepe kuzindua ofisi za chama hicho kata ya Chang'ombe.

Akizungumza na waandishi wa habari katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Dodoma Albert Mgumba amesema idadi hiyo inajumuisha wagombea wote waliochukua fomu katika majimbo 10 yaliyopo mkoani humo.

Amesema pia wapo wanawake waliojitokeza kuwania nafasi hiyo kwenye majimbo ya Kondoa Mjini ambapo kuna mwanamke mmoja, Kondoa vijijini pia amejitokeza mwanamke mmoja, Chemba yupo mwanamke mmoja na Mpwapwa wapo wanawake watatu na kufanya idadi yao kufikia sita.

Majina ya majimbo na idadi ya wanachama waliojitokeza kuchukua fomu kwenye mabano ni Dodoma Mjini (10), Mpwapwa (10), Kibakwe (7), Kondoa Mjini (10), Kondoa Vijijini (15), Chemba (13), Bahi (9), Chilolwa (16), Mtera (10) na Jimbo la Kongwa (9).

Akizungumzia kuhusu kuanza kwa mizunguko ya kura za maoni amesema wameanza leo lakini bado kila halmashauri kupitia kurugenzi yake ya CCM wanajipanga jinsi ya kutumia gari moja badala ya kila mmoja kutumia gari lake.

Ameyataja makundi mengine ndani ya CCM yaliyochukua fomu za kuwania ubunge kuwa ni pamoja na UVCCM (4), UWT (29) na Jumuiya ya Wazazi (4)