
Paul Luziga (17), aliyeongoza Kitaifa matokeo ya Kidato cha Nne ya 2020
Paul ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na EATV na kusema kuwa katika familia yao yeye ni mtoto wa tano na wa mwisho kuzaliwa na kwamba katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, wamekuwa wakilelewa na mama yao pekee baada ya baba yao, Mzee Cosmas Luziga kufariki mwaka 2018.
Paul amesema kuwa akiwa amelala alipigiwa simu na Mkuu wa Shule ya Panda Hill, Zephania Lusanika, akimpongeza kwa kufanya vizuri kwenye matokeo hayo na kuongoza kitaifa jambo ambalo lilimshtua na hakuamini na alidhani anaota.
"Nimefurahi sana japo awali nilikuwa siamini, mama naye amenipigia simu akawa analia huku akinipongeza, kwa kweli nimejisikia vizuri na naamini hii ni changamoto kubwa kwenye maisha yangu ya shule na natamani kuwa Mhandisi", amesema Luziga.
Aidha Paul ameongeza kuwa, anaamini kuwa siri ya kufanya vizuri kwenye mitihani ni kumwamini Mungu, huku akidai kuwa ataendelea kumwamini na kumtumikia katika maisha yake yote pamoja na kuwashukuru walimu wote wa Panda Hill kwa kumuwezesha kufanya vizuri kwenye mitihani yake.
Akielezea elimu yake ya msingi, Paul amesema kuwa alisoma katika Shule ya Msingi Songwe Magereza kwa sababu Baba yake kabla hajafariki alikuwa ni Askari Magereza aliyekuwa anafanya kazi kwenye Gereza la Kilimo la Songwe.