Jumatano , 31st Mei , 2023

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo amewaonya wananchi wa jimbo la Isimani mkoa wa Iringa kuacha kuuza ardhi hovyo badala yake waitumie kuleta tija na kukuza uchumi wao.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo

Chongolo ametoa kauli hiyo kutokana na idadi kubwa ya watu wanaohitaji mashamba kuhamia eneo la Pawaga inakojengwa skimu ya umwagiliaji inayogharimu shilingi bilioni 55, ambapo kumekuwa na wimbi kubwa la wananchi kuuza ardhi bila sababu za msingi. 

"Acheni  kuuza ardhi hovyo ardhi ndio dhahabu ya uhakika, kama unataka fedha mwambie mtu mwaka huu sitaki kushika jembe,lima ardhi yangu hii nipe fedha mwakani nirudishie ardhi yangu ndio mtu mjanja anavyofanya, acheni kuuza ardhi hovyo mtakuja kujuta na mtakuja kulaaniwa na watoto na wajukuu zenu," amesema Chongolo

Amesema mwenye akili haachii ardhi yake kwa ajili ya kumuuzia mtu mwingine anamkodisha ili iendelee kuwa sehemu ya msaada kwake yeye kwa watoto na wajukuu.

"Watu wanapoenda kufuata ardhi vijijini kwani hawajui kama ina tija? hawajui ina faida? hawajui maslahi yake kwani ninyi hamtaki hiyo tija kwanini mnakaa kienyeji, ukinyang'anywa maana yake wewe mwenyewe umeachia achia mambo, simameni mguu sawa lindeni ardhi zenu ziwasaidie badae na watoto wenu," ameongeza Chongolo