Jumanne , 30th Jun , 2020

Ikiwa leo Juni 30, 2020 ni siku ya mwisho kwa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi waliochukua fomu ya kuwania kuteuliwa kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama hicho, Rais Magufuli amerejesha fomu.

Rais Magufuli akipokea baadhi ya fomu za udhamini.

Katika hafla inayoendelea mkoani Dodoma makao makuu ya chama hicho, wenyeviti wa mikoa mbalimbali wa CCM wameeleza idadi ya wanachama waliojitokeza kumdhamini Rais Magufuli.

Jumla ya wanachama 44, 415 wa CCM mkoa wa Dodoma wamemdhamini Mwenyekiti wa CCM Rais John Magufuli katika kuwania urais kupitia CCM.

Aidha Jumla ya wanachama wa CCM  71, 491 kutoka mkoa wa Dar es salaam wamemdhamini Mwenyekiti wa Chama hicho Rais Magufuli katika fomu za kuwania Urais wa Tanzania.

Kwa upande wa mkoa wa Geita jumla ya wanachama 89, 595 wamemdhamini Mwenyekiti wa CCM Rais Magufuli kwenye fomu za kuomba kuteuliwa kuwania nafasi ya Urais wa Tanzania kupitia chama hicho.

Aidha katika mkoa wa Mara jumla ya wanachama 87, 550 wa chama hicho wamejitokeza kumdhamini huku mkoa wa Morogoro wakijitokeza jumla ya wanachama 117, 450.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa CCM Dkt. Bashiru Ally, Jumla ya wanachama Milioni 1,023, 911 wa CCM wamejitokeza kumdhamini Mwenyekiti wao Rais John Magufuli katika fomu za kuwania kupitishwa na chama hicho kugombea nafasi ya Urais kwenye uchaguzi mkuu. Julai 11, Mkutano Mkuu wa chama utakutana kumpigia kura.

Zaidi Tazama Video hapo chini