Jumatatu , 23rd Aug , 2021

Mbunge wa Kawe Josephat Gwajima, amekataa kukaa kwenye kiti pamoja na kutumia kipaza sauti alichoandaliwa alipofika mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge inayoongozwa na Mwenyekiti wake Emmanuel Adamson Mwakasaka, na kuomba vibadilishwe.

Mbunge wa Kawe Josephat Gwajima, alivyowasili kwenye viwanja vya Bunge kuitikia wito wa Spika Job Ndugai

Mbunge huyo wa Kawe Askofu Josephat Gwajima, amechukua hatua hiyo alivyowasili kwenye viwanja vya Bunge hii leo kwa ajili ya kuhojiwa mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ili kujibu tuhuma mbalimbali zinazomkabili, ambapo aliomba kubadilishiwa vitu hivyo.

Mbunge Gwajima aliwasili kwenye viwanja vya Bunge Jijini Dodoma majira ya saa 6:40 mchana kwa ajili ya kuhojiwa ikiwa ni kuitikia wito wa Spika wa Bunge Job Ndugai alioutoa Agosti 21 mwaka huu, ambapo pia kabla ya mahojiano aliomba pia msaidizi wake amletee dawa zake anywe.

Askofu Gwajima alitakiwa kufika mbele ya kamati hiyo kwa mujibu wa Kanuni ya 4 (1) (a) na (b) ya nyongeza ya nane ya kanuni za kudumu za Bunge toleo la Juni 2020 ambayo inaipa mamlaka kamati hiyo kuchunguza mambo yanayohusu maadili ya wabunge yanayopelekwa kwa Spika.