Jumatano , 27th Mar , 2024

Peter Simoni kijana anayekadiwiwa kuwa na umri wa miaka 25 mkazi wa mtaa wa Mkoani Halmashauri ya Mji wa Geita amefariki ghafla wakati akishirikiana na wenzake kuchimba kaburi kwa ajili ya kupumzisha mwili wa Bi Elizabeth Kalamu mwenye umri wa miaka 80 aliyefariki katika mtaa huo 

Inaelezwa kuwa kijana huyo alianguka ghafla na kufariki wakati akiendelea kuchimba kaburi tukio ambalo limezua taharuki kwa wakazi wa mtaa huo.

EATV imefika eneo la tukio na kuzungumza na mashuhuda wa tukio hilo pamoja na viongozi wa eneo hilo wamesema tukio kama hilo la mtu kuanguka ghafla na kufariki kwenye maziko  halijawahi kutokea katika mtaa huo.

“Ameshika tu jembe kwa mara ya kwanza kwamba achimbe ikaonekana kama ameshikwa na hali ya kifafa vile vijana na nzengo yetu wakaamua kumshika na kumuweka pembeni wakijua ile hali itatulia tu na atarudi kwenye hali yake baadae kama dakika moja kumuangalia mwenzetu ndo akawa ametutoka hivyo” amesema George Costantine ambaye ni Katibu wa Maafa Mtaa wa Mkoani

“Tulikuwa ndo tunaanza kuchimba sasa mwezetu akaomba jembe atuoneshe namna ya kuchimba alipoanza namna ya kuchimba pale alikata majembe kama sio manne matano tukaona kama vile kashikwa na kifafa akakauka kama vile anataka kuanguka wakamuwahi wakamshika asije kuanguka” amesema Joseph Elnest ambaye ni Mkazi wa Mtaa wa Mkoani

Kaimu Mganga mfawidhi hospitali ya Halmashauri ya mji wa Geita Thomas Mafuru amekiri hospitali yake kupokea mwili wa kijana huyo kutoka kwa wasamaria wema wakiwa na Polisi  na chanzo cha kifo chake inadhaniwa kuwa ni shambulio la moyo.