Alhamisi , 8th Jan , 2015

Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa imeendelea kubaini na kufichua mapungufu mbalimbali ya kiutendaji katika halmshauri za mkoa wa Dar es salaam.

Mwenyekiti wa Kamati LAAC Mhe. Rajabu Mbarouk Mohamed akiongea na waandishi wa habari

Kamati hiyo imesema utendaji mbovu wa halmashauri nyingi nchini unachangiwa kwa kiasi kikubwa na viongozi wengi wa juu wa halmashauri hizo kutokuwa na madaraka kamili ya kufanya maamuzi.

Akiongea leo wakati kamati hiyo ikifanya ukaguzi katika halmashauri ya manispaa ya Ilala Jijini Dar es Salaam Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Rajabu Mbarouk Mohamed amesema kuwa kamati hiyo imebaini kuwa viongozi 12 wa juu kati ya 20 wa halmashauri hiyo wana kaimu nafasi zao.

Mbarouk ameitaka Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kuwasilisha idadi ya viongozi wa juu wa halmashauri zote nchini wanaokaimu madaraka ifikapo Januari 14 mwaka huu.

Mjumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Mwibara Mhe. Kangi Lugola amesema hali hiyo imeathiri maendeleo ya Halmashauri nyingi nchini licha ya kuwa na vijana wengi wenye uwezo wa kuajiriwa katika nafasi hizo.