Jumanne , 1st Jul , 2014

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini Tanzania LHRC, kimesema mabaraza mengi ya usuluhishi wa migogoro ya ardhi yameshindwa kutatua migogoro hiyo kutokana na mabaraza hayo kutozijua sheria za ardhi.

Mkurugenzi mkuu wa kituo cha sheria na haki za binadamu (LHRC) Bi. Hellen Kijo-Bisimba.

Akizungumza na East Africa Televisheni jijini Dar es Salaam, mkuu wa kitengo cha sheria cha LHRC, wakili Fulgence Masawe amesema mabaraza mengi yamekuwa yakitumia busara zaidi kuliko kufuata sheria hivyo walalamikaji wamekuwa awaridhishi na maamuzi ya mabaraza hayo.

Wakili Fulgence ameitaka Serikali iweke mikakati ya itakayoyajengea uwezo wa kisheria mabaraza hayo ili yaweze kufanya kazi kwa ufasaha ya kutatua migogoro ya ardhi kwa ufanisi zaidi kwa kutoa haki kwa wanaostahili.

Kauli hiyo ya kituo cha sheria na haki za binadamu imekuja wiki chache baada ya mbunge wa Mihambwe Felix Mkosamali kulitaka bunge kutengua sheria ya uundwaji wa mabaraza hayo kwa madai kuwa yameshindwa kuonyesha ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya ardhi.

Sababu nyingine aliyoitaja mbunge huyo ni uchache wa mabaraza hayo, hali ambayo huwalazimu wananchi kusafiri umbali mrefu kwa ajili ya kutafuta haki yao.