Jumatano , 21st Mei , 2025

Mawaziri wa fedha wa nchi zilizostawi kiviwanda duniani za G7 wanakutana nchini Canada kwa mazungumzo yanayojikita katika mzozo wa Ukraine na kuyumba kwa uchumi wa dunia kulikosababishwa na ushuru uliowekwa na rais wa Marekani Donald Trump.

Katika mikutano itakayoendelea hadi kesho Alhamisi viongozi watajadili hali ya uchumi wa dunia na kutafuta msimamo wa pamoja kuhusu suala la Ukraine ambayo inawakilishwa na waziri wake wa fedha Sergii Marchenko.

Waziri wa fedha wa Canada Francois-Philippe Champagne amewaambia waandishi habari kwamba uwepo wa Ukraine katika mkutano huo unatoa ujumbe mzito kwa ulimwengu kwamba nchi wanachama wa G7 wanaahidi tena kwa dhati kuisaidia Ukraine dhidi ya uvamizi wa Urusi. 

Akiwa ameandamana na waziri wa fedha wa Ukraine, waziri huyo pia amesema watajadili jinsi ya kuijenga upya Ukraine.