Jumamosi , 13th Mei , 2023

Waziri wa Maliasili Mohamed Mchengerwa na RC Mbeya wamefika Kijiji cha Mwanavala wilayani Mbarali kutokana na agizo la Waziri Mkuu la kuwataka kufika ili kuona hali ya ugomvi uliotokea baina ya wananchi na Askari wa TANAPA na kubaini hakuna vifo wala mifugo iliyoshikiliwa ama kuuawa.

Waziri wa Maliasili na Utalii Mohamed Mchengerwa, akiwa na viongozi wengine alioambatana nao

Hoja hiyo ya vurugu kati ya wananchi na wahifadhi wa TANAPA iliibuliwa na Mbunge wa Mbarali, Fransis Mtega, aliyeomba kutoa hoja ya dharura  ya kulitaka Bunge lijadili suala hilo na ndipo Waziri Mkuu alipotoa maelekezo.

"Nimesikitishwa na kauli za Mbunge malalamiko na shutuma zake zimeleta taharuki ambayo sijaikuta eneo hili na wananchi wamekiri kuingia ndani ya eneo hili na  wameiomba serikali kuharakisha  mchakato wa kuwatafutia  maeneo ya kuishi" amesema Waziri Mchengerwa

Ametaja baadhi ya  tuhuma ambazo hazina ukweli  na ambazo zimethibitishwa na wananchi wenyewe kuwa si kweli ni pamoja na wananchi kukataa kuwa hakuna mifugo iliyochukuliwa na wahifadhi 230  kama ilivyoripotiwa na Mbunge zaidi ya purukushani ya Mbwa wakali wa wananchi husika na wahifadhi.

Aidha, amewaonya  viongozi wa kisiasa kuacha kuwachonganisha wananchi na serikali yao ambapo amesisitiza kuwa wananchi ni wahifadhi namba moja.

Amemwelekeza Katibu Mkuu wa Maliasili kuchukua hatua dhidi ya askari waliohusika kuwachapa wananchi husika, na  ametoa mkono wa pole wa shilingi milioni moja kwa wananchi watano kila moja  kama kifuta machozi kwa wahusika.

Kwa upande mwingine Mhe. Mchengerwa amekutana  na Uongozi mzima  wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Mbarali ukiongozwa na Mwenyekiti wa Wilaya, Katibu na Makatibu wote wa Kata na matawi wa CCM wilaya ya Mbarali na amewaomba waendelee kuwa karibu na wananchi na kutoa elimu ya uhifadhi huku akisisitiza kuwa hifadhi zote ni za wananchi na wananchi  ndiyo msingi wa nchi yoyote duniani.

Mkuu wa mkoa wa Mbeya ambaye pia aliambatana katika ziara hiyo na kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa na wilaya ya Mabarali na viongozi wa CCM wa wilaya hiyo aliwaambia wananchi katika mkutano huo kuwa serikali itahakikisha kuwa wananchi wote wanatendewa haki ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini za makazi na kuwalipa fidia stahiki.