Jumatano , 6th Dec , 2017

Mbunge wa CHADEMA jimbo la Ubungo Saed Kubenea, amekanusha juu ya kauli zinazomkabili zikisema anahama chama hicho na kuhamia Chama cha Mapinduzi (CCM).

Mbunge huyo amesema hajawahi kuzungumza na chombo chochote cha habari juu ya kuhamia CCM , wala kuwa na wazo la kuitema  CHADEMA.

“Sioni jipya ambalo linanifanya nishawishike kuhamia CCM , nimekuwa nikiandika habari za uchunguzi kwa zaidi ya miaka 15, nimekua mkosoaji juu ya chama tawala dhidi ya rasilimali za nchi” Amesema Kubenea

“Mimi sinunuliki, nimepitia vikwazo vingi na vishawishi vya fedha wala sijateteleka, mimi sina bei na kama nikiondoka nitaondoka bila bei  ” Amesema

Amesema kwa magazeti yote yaliyoandika habari zake siku ya leo, watambue yeye ni Mbunge wa CHADEMA hadi mwaka 2020.

Hatua hii ya Kubenea, imekuja baada ya kuibuka wimbi la viongozi wa siasa kuhamia chama tawala , wakidai wanaunga mkono juhudi za Rais John Pombe Magufuli kwa kuinua nchi  uchumi  pamoja na  biashara.