Jumatano , 8th Jun , 2016

Serikali imesema haitatoa kazi tena kwa kampuni za makandarasi wa barabara watakaobainika kufanya kazi chini ya kiwango na kuisababishia hasara serikali.

Prof. Makame Mbarawa (alienyoosha kidole), akiwa katika moja ya ziara zake za Ukaguzi wa Ujenzi wa Barabara.

Akizungumza katika ziara yake ya kukagua barabara kuu ya Tanzania-Zambia (Tanzam) kipande cha Mafinga hadi Igawa Mkoani Mbeya, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa amesema serikali haitavumulia watu hao kwa kuwa wanatumia fedha za wananchi.

Akiongea na wawakilishi wa Makandarasi kutoka kampuni ya China Civil Engineering Contractors, amewaambia kwa serikali haitavumulia kuona kazi hiyo inalipuliwa hivyo hawana budi kujenga kwa kiwango kinachohitajika.

Aidha, Waziri Mbarawa aliwataka wananchi kuwa walinzi wa miundombini inayojengwa na serikali badala ya kuihujumu na kuonya kuwa hatua kali zitachukuliwa kwa yeyote atakaekamatwa akiharibu miundombinu hiyo.

Prof. Mbarawa amesema kukamilika kwa barabara hiyo kutasaidia kupunguza ajali za barabarani kwa sababu awali ilikua na upana wa Mita nane lakini baada ya ujenzi huo itakua Mita 12.