Jumapili , 26th Jul , 2020

Aliyewahi kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dkt Hellen Kijo Bisimba, amesema kuwa wakati wa uongozi wake Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Marehemu Benjamin William Mkapa alikataa kabisa kuitwa jina la mtukufu.

Dkt Hellen Kijo Bisimba.

Dkt KijoBisimba ametoa kauli hiyo wakati akizungumza kwenye kipindi cha SupaBreakfast ya East Africa Radio, wakati akieleza ni kwa namna gani anamfahamu na atamkumbuka Rais Mkapa.

"Ninachokikumbuka kwa Marehemu Rais Mkapa mwaka 1995, alivyoingia madarakani alikataa kabisa kuitwa mtukufu" amesema Dkt Kijo Bisimba.

Aidha Dkt Kijo Bisimba ameongeza kuwa, "Katika kipindi cha uongozi wake ndio Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Tanzania kilianzishwa na mimi nikawa Mkurugenzi wa kwanza mwaka 1996, hivyo Mkapa ni mtu aliyejali sana haki za binadamu''.

Rais wa Awamu ya Tatu Benjamin William Mkapa, alifariki Dunia usiku wa kuamkia Julai 24, 2020, katika moja ya Hospitali zilizopo Jijini Dar es Salaam, na atazikwa siku ya Jumatano ya Julai 29, 2020, Kijijini kwao Lupaso mkoani Mtwara.