Jumanne , 19th Jan , 2016

Shirika la Umeme Tanzinia (TANESCO) mkoani Mtwara limefanikiwa kumkamata Jema Khamisi, mkazi wa kata ya Chikongola manispaa ya Mtwara kutokana na kubaini kuwa anatumia umeme wa wizi kwa muda ambao haukuweza kubainika haraka.

Moja ya nyumba ambayo Mwenye Nyumba amejiunganishia umeme wa wizi katika nyumba yake

Hatua hiyo imetokana na shirika hilo kupitia maofisa wake kuendesha oparesheni ya kufanya ukaguzi wa kushtukiza kwa wateja wake, wakiambatana na Mhandisi wa shirika hilo mkoa wa Mtwara Daniel Kyando, iliyofanyika katika maeneo mbalimbali ya manispaa ya Mtwara Mikindani.

Akitoa utetezi wake baada ya kukamatwa, Jema, ambaye katika nyumba hiyo anaishi na mume wake Hamisi Namwelenu, ambaye hata hivyo hakuweza kupatikana kwa madai kuwa alikuwa kwenye majukumu yake ya kila siku, amesema hajui lolote kwani toka wamefunga mita ya Luku hakuwahi kuingiza umeme na baadala yake jukumu hilo linatekelezwa na mume wake.

Kwa upande wake, mhandisi wa mkoa, Daniel Kyando, amesema kwa mujibu wa sheria za nchi, kitendo hichi ni kosa kisheria na kwamba kwa taratibu za TANESCO muhusika anapaswa kuchukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani.