Ijumaa , 23rd Aug , 2019

Mtoto wa Darasa la nne katika Shule ya Msingi  Osanyui aitwaye Elibariki Lekine, mkazi wa Murieti Mkoani Arusha, amekutwa amefariki dunia kwa kujinyonga kwa kutumia kamba ya katani katika nyumba ambayo inaendelea na ujenzi.

Taarifa hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha ACP Jonathan Shana, ambapo amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa, mtoto huyo kabla ya kufariki alikuwa na ugomvi na Baba yake Mzazi.

''Ugomvi ulikuwa  unatokana na marehemu kutotaka kwenda shule, inaonekana kwamba marehemu alikuwa mtoro sugu, hili nimpongeze baba yake kwa kuhakikisha kwamba mtoto anaenda shule, na mwezi mmoja au miwili iliyopita mzazi wake alijaribu  kumpeleka kwa ndugu zake ambao ni wakali zaidi lakini pamoja na hayo mtoto akawa bado hataki, nadhani baada ya mtoto kuona kabanwa kila pembe akaamua kuutoa uhai wake'' amesema RPC Shana.

Ndani ya Juma moja Mkoa wa Arusha umekumbwa na matukio mawili ya watoto ambao ni wanafunzi kujichukulia sheria mkononi ambazo zinagharimu uhai wao.

Jumapili iliyopita mwanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Arusha Meru Faisal Salimu Ibrahim (19), alijiua kwa kujipiga risasi moja kichwani katika paji la uso katika chumba chake kwa kutumia bunduki aina ya Rifle Winchester inayomilikiwa na Baba yake aitwaye Salim Ibrahim (56yrs).