Ijumaa , 6th Nov , 2015

Mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Joseph Bagule (61) mkazi wa Kilimahewa kata ya maili moja mjini Kibaha, anatuhumiwa kuwafungia watoto yatima ndani na kumuweka kinyumba mjukuu wake wa miaka 16 na mtoto wa dada yake (25) na kuzaa nao watoto.

Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jafari Ibrahimu

Kamanda wa Polisi mkoani Pwani Jafari Ibrahimu amekiri kuwepo kwa tukio hilo na kuwa mtuhumiwa anashikiliwa na polisi kwa uchunguzi zaidi na pia kufanya vipimo vya DNA kwa ajili ya kupata uhakika kama ni kweli mtoto huyo anayedaiwa kuzaa na mjukuu wake ni wake.

Kamanda Jafari amesema kuwa inadaiwa mchungaji huyo aliwafungia watoto hao ndani na kuwanyima haki yao ya msingi ikiwemo kwenda shule kwa madai kuwa dini hairuhusu watoto kusoma.

Inadaiwa familia ya mchungaji huyo ni ya watu 14, watoto wakiwa ni 9 ambao wanne wamefikisha umri wa kwenda shule na hawajaandikishwa kwa upande wa watu wazima ni watano.

Aidha taarifa kutoka kwa majirani kwa mzee zimebainisha kuwa Mzee huyo ambaye anajifanya mchungaji huendesha ibada kifamilia na hairuhusiwi watu wa nje kushiriki ibada hiyo ambayo imepewa jina la IBADANI.

Wakiongea na waandishi wa habari wakazi wa mtaa wa kilimahewa walisema wamekuwa wakishangazwa na nyendo za mchungaji huyo kwa kipindi kirefu baada ya kuona mambo yasiyo ya kawaida yakifanyika katika nyumba yake ambayo ndio anayotumia kama kanisa.

Kwa upande wake Mzee Bagule akihojiwa na waandishi wa habari mbele ya afisa mtendaji wa mtaa na polisi alikana tuhuma hizo na kusema inashindwa kuwapeleka watoto hao shule kutokana na ugumu wa maisha na wale ambao amewasomesha wanatosha.